muhtasari

Home » , , , » MAANDAMANO YA VYAMA VYA UPINZANI YASITISHWA...KWANINI SOMA UJIONEE...

MAANDAMANO YA VYAMA VYA UPINZANI YASITISHWA...KWANINI SOMA UJIONEE...


Viongozi Wakuu wa vyama vya siasa nchini Tanzania, NCCR-Mageuzi, CHADEMA na CUF wametangaza kusitisha mpango wa maandamano uliokuwa umepangwa kufanyika siku ya Alhamisi, Oktoba 10, 2013 katika maeneo ya mikoa ya Unguja, Dar es Salaam, Mbeya, Kigoma, Dodoma, Tanga, Mwanza na Arusha kwa lengo la kudai upatikanaji wa muafaka wa mchakato wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba yatakayowezesha kuundwa kwa Katiba Mpya inayokubalika na wananchi.

Mwenyekiti wa CUF akizungumza kwa niaba ya viongozi wenzake katika ofisi za Makao Makuu ya NCCR-Mageuzi jijini Dar es Salam, Profesa Ibrahim Lipumba amesema sababu kubwa ya kusitisha mikutano iliyopangwa inatokana na kuitambua nia ya Rais Kikwete aliyoionesha katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi, ambapo alibainisha wazi kuwa atakutana na viongozi wa vyama hivyo  kuzungumzia suala hilo la Muswada wa Katiba.
 

Kutokana na nia hiyo, alisema vyama hivyo havina budi kusubiri mazungumzo na Rais Kikete yatakayotoa dira ya kitakachoendelea katika lengo la kupata katiba shirikishi na inayokubalika na raia wengi.

“Tumesikia kupitia vyombo vya habari ambavyo navyo vimenukuu taarifa kutoka Ikulu, inayobainisha kuwa Rais Jakaya Kikwete amepanga kukutana na viongozi wa upinzani kati ya Oktoba 13 na 15 ili kujadili na kupata muafaka wa suala hili la Katiba. 


"Tunaamini kuwa taarifa hizi ni sahihi kabisa, hivyo tumeamua kusitisha maandamano yetu, yaliyolenga kushinikiza nguvu ya umma kuungana nasi katika kudai mchakato wa kuipata Katiba shirikishi, na kushinikiza Rais kutosaini kabisa muswada huo wa sheria  kwa kuwa una upungufu,” alisema Profesa Lipumba.

Viongozi hao pia wamesema wapo tayari kusubiri kukutana na Rais katika tarehe itakayopangwa na kuafikiwa.

“Pamoja na kuahirisha maandamano haya, tunapendekeza huo mkutano ulioahidiwa na Rais, ufanyike mapema ili mchakato wa Katiba unaosuasua kwa sasa uendelee kwa ufanisi,” alisema Lipumba.

Ikiwa mazungumzo hayo hayatafanikiwa, viongozi hao wameahidi kurejesha ratiba ya maandamano na mikutano.

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger