muhtasari

Home » , » MAKANDARASI HATARINI KUGOMA...KISA UKATA WA TANROADS...

MAKANDARASI HATARINI KUGOMA...KISA UKATA WA TANROADS...



Rais Jakaya Kikwete (aliyeshika mkasi) akikata utepe kuzindua rasmi ujenzi wa barabara ya Kagoma-Lusahunga katika wilayani Biharamulo. jana alielezwa kuwepo kwa mgomo wa makandarasi kwa sababu bado hawajalipwa fedha zao za ujenzi
Rais Jakaya Kikwete amezindua ujenzi wa barabara, huku akielezwa kuwa zaidi ya makandarasi 30 nchini ambao wanajenga barabara kwa fedha za ndani wako mbioni kugoma kuendelea na ujenzi huo kutokana na Wakala wa Barabara (Tanroads) kukosa fedha za kuwalipa kwa wakati.
Rais Kikwete yuko katika ziara ya kutembelea Mkoa wa Simiyu aliouzindua jana na kusema ameunda mikoa mipya kwa ajili ya kurahisisha utekelezaji wa shughuli za maendeleo. Mikoa mingine iliyoundwa ni; Njombe, Geita na Katavi.
Akizungumza mbele ya Rais Jakaya Kikwete, wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la Ujenzi wa Barabara ya lami ya Bariadi hadi Lamadi yenye urefu wa kilomita 71.8, Mtendaji Mkuu wa Tanroads, Patrick Mfugale alisema ni muda mrefu sasa fedha zimekuwa zikichelewa kufika kwa wakati kwao, hivyo kushindwa kuwalipa makandarasi na wametishia kugoma kuendelea na kazi ya ujenzi.
Alisema kuchelewa kwa fedha hizo kunakwamisha ujenzi wa barabara hizo ikiwa ni pamoja na kuitia hasara serikali kutokana na kulazimika kulipa riba na fidia ya hasara kutokana na kuchelewa kulipa kwa wakati.
Rais Kikwete alisema atafuatilia suala hilo ikiwa ni pamoja na kuwahimiza wanaohusika na fedha kuhakikisha zinapatikana haraka na hivyo kuwaondoa wasiwasi Waziri wa Ujenzi pamoja na makandarasi.
Awali kabla ya kumkaribisha Rais Kikwete kuzungumza na wananchi, Waziri wa Ujenzi,John
Magufuli alieleza kuwa katika barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 71.8 Serikali imegharimia fedha zote kiasi cha Sh70.9 bilioni.
Alisema katika mradi huo, Serikal imelipa fidia ya Sh795 milioni kwa wananchi ambao walifuatwa na barabara, lakini pia imeweza kubomoa nyumba kwa wale ambao walijenga barabarani.
Azindua Benki ya Wananchi Simiyu
Katika ziara hiyo jana, Rais Kikwete alizindua Benki ya Wananchi wa Simiyu na kuwataka wananchi kutunza fedha zao katika benki hiyo kwa vile kufanya hivyo kutasaidia kupanga mipango ya kiuchumi. Alisema benki ni kichocheo cha uchumi na kwamba ili iweze kuwa na maana ni lazima wananchi waitumie benki hiyo kwa kuweka fedha na kukopa.
Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Benki hiyo, Mhandisi Christopher Sayi akitoa taarifa kwa Rais Kikwete alisema benki hiyo itachochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo kwa kutoa huduma za kifedha, mikopo yenye masharti nafuu na fursa ya kuwekeza mitaji yao.
Alieleza kuwa mchakato wa kuanzisha benki hiyo unaoratibiwa na kamati maalumu, umeisha kusanya mtaji wa Sh1.8bilioni na kukamilisha taratibu za kibenki, na kwamba, wanatarajia kufungua milango na kuanza kutoa huduma Februari mwakani.
-MWANANCHI

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger