muhtasari

Home » , » HATARI…MAUAJI YAITIKISA NCHI...JAMBAZI LAENDESHA MAUAJI YA WATU 8 KWA SIKU TATU MFULULIZO, IGP MANGU ASHTUSHWA, APELEKA WAPELELEZI KUMSAKA…

HATARI…MAUAJI YAITIKISA NCHI...JAMBAZI LAENDESHA MAUAJI YA WATU 8 KWA SIKU TATU MFULULIZO, IGP MANGU ASHTUSHWA, APELEKA WAPELELEZI KUMSAKA…


Mauaji ya kutisha yametikisha wilaya ya Tarime kiasi cha kumfanya Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu, kutuma timu maalum kutoka makao makuu ya jeshi hilo inayohusisha kamisheni ya Operesheni kufanya uchunguzi.

Hatua ya kupelekwa kwa timu hiyo inatokana na mauaji ya mfululizo katika mji wa Tarime ambayo ipo kwenye himaya ya Kanda Maalum ya Polisi ya Tarime na Rorya ambayo yametokea kwa watu wanane katika kipindi cha siku tatu.

Mauaji hayo yanadaiwa kufanywa na jambazi mwenye silaha katika mji wa Tarime mkoani Mara kwa siku tatu kuanzia Jumatatu hadi jana.

Mmoja wa watu waliouawa ni askari mstaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Koplo Zakaria Chacha Mwita ambaye ni mtoto wa marehemu Meja Jenerali Mwita Marwa.

Pia wamo aliyekuwa Mhandisi Ujenzi Wilaya ya Rorya, aliyetajwa kwa jina la David Mwasi Misiwa.

Wengine ni mfanyabiashara, Samuel Richard Mohenga na huku Jeshi la Polisi likisema kuwa linaendesha msako.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Tarime/Royra, Justus Kamugisha, alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kusema kuwa mtu anayesadikiwa kuwa jambazi akiwa na bunduki kwa siku tatu kuanzia Januari 26, mwaka huu usiku aliua watu saba kwa kuwapiga risasi  na kujeruhi kadhaa.

Aliwataja wengine kuwa ni mwendesha bodaboda, mkazi wa kijiji cha Nkende, Juma  Marwa Nyaitara, Erick Lucas Makanya, mfanyabiashara  wa bucha mkazi wa kijiji cha Rebu, Juma Mwita Mroni na mkazi wa kijiji cha Kenyamanyori, Robert Chacha Kisiri.

Jana asubuhi, wakazi wa mji wa Tarime na vitongoji vyake walimfananisha mtu aliyekuwa amevaa koti refu na mtuhumiwa wa mauaji hayo na kutaka kumshushia kipigo, lakini aliokolewa na polisi waliorusha risasi hewani na kumpeleka katika kituo cha polisi.

Kamanda Kamugisha aliwashauri wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa mara watakapomuona mtuhumiwa.

 Alisema polisi wanafanya msako katika vijiji vya Kenyamanyori, Rebu, Nkende, Mogabiri na Kibumaye katika kata za Kitare, Turwa na Binagi kwenye Tarafa ya Inchage.

Mkuu wa Mkoa wa Mara, John Tuppa na Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele wakishirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Tarime jana  walitembelea maeneo ya vijiji ambavyo wakazi wake wameuawa na jambazi hilo.

TIMU YA MAKAO MAKUU
Alizungumzia timu iliyotumwa Tarime, Mkuu wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi nchini, Kamishna Paul Chagonja, alisema kuwa ni ya wapelelezi na Intelijensia na inakwenda kuongeza nguvu katika juhudi zinazofanywa na mkoa wa Mara kuhakikisha jambazi huyo anakamatwa ili kuondoa hofu kwa wananchi.

Chagonja alisema juhudi za kumsaka jambazi huyo zinaendelea kufanywa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

SOPHIA SIMBA ALAANI MAUAJI
Wakati huo huo, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba,  amelaani maauji ya wanawake watano waliotaarifiwa kuuawa katika wilaya za Musoma, Butiama na Rorya mkoani Mara.

Alisema wizara inasisitiza kuwa mtazamo huo ni hasi na unakwenda kinyume cha haki za binadamu hivyo jamii haina budi kuachana na imani zinazosababisha mauaji.
 
“Wizara inahimiza wananchi kupinga dhana potofu zinazopelekea mauaji ya wanawake ikiwa ni pamoja na imani za kishirikina, uchu wa kupata utajiri wa haraka, kulipiza kisasi na kuendeleza hulka ya ukatili katika jamii,” alisema.

Alisema: “Mauaji dhidi ya wanawake yanapotokea katika jamii zetu yanarudisha nyuma juhudi za serikali katika kuzuia ukatili dhidi ya wanawake katika jamii kutokana tu na tofauti za kimaumbile.
 
Wizara inaitaka jamii itambue kuwa wanawake wana haki ya kuthaminiwa utu wao na kushiriki haki zote za msingi bila ubaguzi wowote ambao unaweza kuhatarisha haki yao ya kuishi ambayo ndiyo haki kuu kuliko haki zote,” alisema na kuongeza:

“Kushamiri kwa mauaji ya kikatili wanayofanyiwa wanawake katika wilaya za mkoa wa Mara ni jambo ambalo linasababisha hofu kubwa miongoni mwa wanawake. Mauaji hayo yanawakosesha amani na utulivu na hivyo kuzorotesha ari yao katika shughuli za uzalishaji mali.”

CHANZO: NIPASHE

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger