muhtasari

Home » , » KATIBA MPYA:LOWASSA AGEUKWA...

KATIBA MPYA:LOWASSA AGEUKWA...


Edward Lowassa akisimikwa Utemi

WAKATI mchakato wa Katiba Mpya ukitajwa kutaka kuhujumiwa na moja ya mitandao ya urais katika Chama cha Mapinduzi (CCM) ili pamoja na mambo mengine kumkomoa Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amegeukwa huku watu wanaodhaniwa kumuunga mkono kisiasa wakiumbuliwa na wenzao.
Lowassa amegeukwa baada ya kutolewa kwa tamko kupinga kitendo chake cha kufanyiwa mila za kijadi (tambiko) na wana-ukoo wa Mtemi wa Unyanyembe, ukoo unaohusishwa na Waziri wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta.
Kwa mujibu wa tangazo rasmi lililochapishwa katika gazeti hili, Septemba 14, mwaka huu, Lowassa ambaye anatajwa kuweza kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, alifanyiwa mila za kijadi (tambiko) akipewa heshima ya kuwa chifu wa Wanyanyembe, jambo ambalo sasa linadaiwa kufanyika bila ridhaa ya wanaukoo husika.
Kutokana na hali hiyo, tamko rasmi la Wanyanyembe la kupinga na kulaani tukio hilo limetangazwa huku sehemu yake kubwa likimpigia chapuo Waziri wa Afrika Mashariki, Sitta, ambaye awali, baada ya Lowassa kupewa hadhi ya chifu wa Wanyanyembe, taarifa zilisambazwa kwamba ameisambarartisha moja ya ngome za Waziri Sitta.
Hali hiyo ya siasa za ndani ya CCM kupenyezwa katika koo za kichifu inaandika historia mpya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, ikitabiriwa ya kwamba vituko zaidi vinaweza kuibuka na hasa ndani ya CCM, chenye jukumu la kuteua mgombea wake wa urais katika mazingira ya siasa za ushindani ambazo mara kwa mara, zimekuwa zikitawaliwa kwa mizengwe na hila.
Ili kuthibitisha msuguano wa kisiasa unaovuka mipaka ya vyama ambao sasa unazama katika koo za kichifu, tamko hilo la Wanyanyembe linaeleza: “Kusema Mhe. Lowassa Mbunge wa Monduli kavunja ngome ya Mhe. Samuel Sitta ni utashi wa kijinga. Mhe. Samuel Sitta ni Mnyanyembe na jina lake kwa upande wa Utemi anaitwa Ifuma, Itetema ni kwake. Babu yake wa kumzaa mama yake Hatat Kagoli Said Fundikira, wajomba zake Mtemi Nassoro S. Fundikira, Mtemi Abdallah S. Fundikira, mama, wajomba zake wamezikwa Itetema.”
Lowassa ambaye alijiuzulu Uwaziri Mkuu mwaka 2008, kwa kuhusishwa na kashfa ya mradi wa umeme uliokabidhiwa kampuni ya Richmond Development LLC, hakuwa tayari kuzungumzia hatua hiyo ya kugeukwa.
Raia Mwema ilimtafuta Lowassa kutaka kujua ni namna gani aliweza kupewa hadhi ya uchifu wa Unyanyembe katika mazingira hayo tata na kama kweli kuna nguvu ya fedha ilitumika ili kufanikisha tukio hilo lakini Lowassa alipopatikana kwa simu alijibu; “Nipo nje ya nchi,” Na kukata simu.
Hujuma ya Katiba Mpya CCM
Katika hatua nyingine, zimekuwapo habari kwamba ndani ya CCM kumekuwapo na kundi maalumu lenye malengo ya kukwamisha mchakato wa Katiba Mpya ili hatimaye Katiba ya sasa iendelee kutumika katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kutokana na maandalizi yao kuingiliwa ikiwa kutakuwapo na serikali tatu.
Inaelezwa kwamba kundi hilo ambalo tayari lina mgombea wake wa urais ambaye amefanikiwa kujenga mtandao ndani ya CCM, serikalini na kwa baadhi ya wadau wakuu wa sekta binafsi, linapigania kuendelea kutumika kwa Katiba ya sasa katika uchaguzi ujao wa mwaka 2015 kwa sababu kukubali Katiba Mpya maana yake ni kuvuruga mtandao wao wa urais, ili hali muda waliotumia kujenga mtandao huo ni mrefu na uliogharimu fedha nyingi.
Chanzo chetu cha habari kutoka CCM kinaeleza kwamba mtego mkubwa wa kundi hilo umewekwa katika Bunge la Katiba ambamo kati ya wajumbe wanaounda Bunge hilo ni wabunge wa CCM ambao wengi wamo katika kundi hilo na wanamuunga mkono mgombea huyo anayetajwa kutokea mikoa ya Kanda ya Kaskazini mwa nchi.
“Bado kuna kilio kwamba mchakato huu wa Katiba Mpya si wazo la Chama cha Mapinduzi bali ni mchakato binafsi wa Rais Kikwete, na utaona alitangaza kuanza kwa mchakato huu kabla ya kukishirikisha chama chake. Na hili lilijitokeza katika kikao cha wabunge wa CCM hivi karibuni mjini Dodoma, wapo waliodiriki kusema Katiba Mpya haimo katika Ilani ya CCM na kwa hiyo jambo la muhimu kwao ni kutekelezwa kwa Ilani ya Uchaguzi,” kinaeleza chanzo chetu cha habari ndani ya CCM.
Kundi hilo linaanza kubainika katika wakati ambao tayari Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe akishinikiza mchakato huo wa Katiba usonge mbele na kama Rais Kikwete asiposaini Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, atamshangaa na kimsingi, Rais anaweza kuingia katika mgogoro na Bunge.
Lakini wakati Waziri Chikawe akisema hayo, chanzo chetu kingine cha uhakika cha habari kinaeleza kwamba uongozi wa CCM kwa sasa, chini ya Katibu Mkuu, Abdulrahaman Kinana, hautaweza kumudu kuwatuliza wabunge wa chama hicho kama ikitokea Rais Kikwete hatosaini muswada huo.
Kutokana na hali, taarifa za uhakika zinaeleza kwamba Rais Kikwete ambaye amerejea nchini Jumatatu wiki hii, atasaini muswada huo lakini pia ili kutuliza msuguamo kuhusu Katiba Mpya na hasa wakati huu wa kuelekea katika Bunge la Katiba, muswada huo baada ya kusainiwa na Rais na kuwa sheria, sheria hiyo itarudishwa bungeni kufanyiwa marekebisho madogo.
Kati ya marekebisho madogo yanayoweza kupendekezwa kufanyika katika mkutano ujao wa Bunge unaotarajiwa kufanyika Oktoba 15, mwaka huu kabla ya kuitishwa kwa Bunge la Katiba Novemba, mwaka huu, ni pamoja na kuiongezea uhai Tume ya Mabadiliko ya Katiba inayoongozwa na Jaji Joseph Warioba, ili iwepo hadi wakati wa mchakato wa kura za maoni kuhusu Katiba Mpya.
Hata hivyo, wakosoaji wa kuendelea kuwapo kwa Tume hiyo wamekuwa wakieleza kwamba hawaoni mantiki ya Tume hiyo kuendelea kuwapo kwa sababu wakati wa kura ya maoni, wananchi wataulizwa swali na kujibu Ndiyo au Hapana, na jibu lolote kati ya hayo ni jibu sahihi, na wanahoji Tume iwepo ili kufanya nini?
Pia wakosoaji hao wanasema kiutaratibu Tume za Rais humaliza muda wake baada ya kukabidhi ripoti kuhusu kazi waliyopaswa kuifanya, wakirejea Tume mbalimbali za Rais, kuanzia ile ya Jaji Francis Nyalali na nyinginezo.
Mawaziri wajibu mapigo ya wapinzani
Katika hatua nyingine, Mwandishi Wetu Mary Victor, anaripoti kwamba, mawaziri watatu wa serikali ya Rais Kikwete wamejibu makombora waliyotupiwa na vyama vya upinzani – wakisema hawana mpango wowote wa kujiuzulu kama wanavyoshinikizwa.
Mawaziri hao ni Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu) , Stephen Wassira , Waziri wa Katiba na Sheria , Mathias Chikawe na Waziri wa Maendeleo ya Jamii , Jinsia na Watoto, Sophia Simba.
Vyama vya upinzani vilidai kwamba mawaziri hao wanapaswa kujiuzulu kutokana na msimamo wao wa kumtaka Kikwete asaini  Muswada wa Marekebisho ya Katiba unaopingwa na vyama hivyo kwa ajili ya kuepusha kuvunjika kwa Bunge.
Katika mazungumzo waliyofanya na gazeti hili kwa nyakati tofauti wiki hii, mawaziri hao walisema hawajafanya jambo lolote kinyume cha utaratibu na madai ya kuwataka wajiuzulu hayana maana yoyote.
Kwa upade wake, Wassira alisema; “Nijiuzulu kwa lipi haswa? Kwa sababu nina mawazo tofauti na wapinzani? Yaani nchi hii siku hizi ukiwa na mawazo tofauti na wapinzani basi ujiuzulu. Mimi nasema, basi na wao wajiuzulu kwa sababu wametofautiana na mimi.
“Jambo la msingi ambalo nataka kuliweka wazi hapa ni kwamba wapinzani walipoteza haki ya kuupinga huu muswada mara baada ya kuamua kukimbia bungeni. Pale ndipo mahala pekee ambako sheria zinatungwa.
“Sheria hazitungwi Ikulu wala kwenye viwanja vya Jangwani. Sasa wao sehemu halali ya kutunga sheria wanazira halafu wanataka sheria zikatungwe na Rais Ikulu au na wananchi pale Jangwani. Haiwezekani, alisema mwanasiasa huyo mkongwe.
Kwa upande wake, Chikawe alisema kwa ufupi, “Siwezi kujiuzulu kwa sababu ya kusema  ukweli. Hivi Rais akiusaini muswada huo watamtaka ajiuzulu pia? Siwezi kujiuzulu  kwa sababu ya kusema ukweli. Naijua katiba na nakijua kifungu hicho, wakiseme chote vizuri wasiwapotoshe ninyi na wananchi.”
Kifungu anachokizungumzia Waziri ni kile kilichozungumzwa na Mbunge wa Ubungo (CHADEMA) na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa chama hicho, John Mnyika aliyesema ““Wassira, Chikawe na Simba kama wana hofu kwamba Bunge litavunjwa iwapo muswada utarejeshwa mara ya tatu na wao watapoteza nafasi zao za uwaziri.”
Naye Sophia Simba alipoulizwa na Raia Mwema  ikiwa  yupo tayari kujiuzulu, alisema “Hao wapinzani wanachanganyikiwa . Mimi sijazungumzia hayo . Mimi nilizungumza kuhusu kauli ya Mbowe ya kuitaka jamii kutotii sheria. Hao hawastahili kuitwa viongozi kwani wanachochea fujo ndani ya jamii”
Msimamo wa vyama hivyo kumtaka Rais asiusaini muswada, umetokana na baadhi ya vifungu kuingizwa kinyemela kwenye muswada uliowasilishwa bungeni na pia madai kwamba mchakato mzima umehodhiwa na CCM. 
-RAIA MWEMA

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger