muhtasari

Home » , » Operesheni Kimbuga yadaiwa kukwepa wababe...

Operesheni Kimbuga yadaiwa kukwepa wababe...




·         Msemaji akanusha na kuahidi mafanikio zaidi
ZIKIWA zimebakia wiki tatu kukamilika kwa awamu ya pili ya operesheni Kimbunga dhidi ya wahamiaji haramu, ziko dalili za kushindwa kuwakamata wahamiaji haramu wafugaji wanaotuhumiwa kuharibu mazingira kutokana na wingi wa mifugo yao.
Taarifa kutoka ndani ya wana-operesheni hiyo na Serikali ya Mkoa wa Kagera zinaeleza kuwa operesheni hiyo inapambana na ugumu katika kuwakamata wafugaji hao matajiri kwa sababu imedhihirika kuwa wana vibali vya uraia.
Kwa mujibu wa mmoja wa maofisa anayeshiriki katika operesheni hiyo ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini, imedhihirika kwamba watu hao walipewa uraia bila kwanza kuukana uraia wa nchi zao kama sheria  inavyotaka, hali inayowafanya kuwa raia wa nchi mbili, wakiwa Tanzania wanakuwa raia na wakiwa kwao ni raia, na  wakati huu wa operesheni wote wamekimbilia nchini Rwanda.
"Ili tufanikiwe kukomesha hali hii ninachoweza kushauri ni kumuomba Rais au baada ya operesheni hii ashauriwe kubatilisha hati za uraia wao, ili tuwafanyie uchunguzi makini kulingana na mienendo yao kabla ya kuwapa uraia tena na wakubali kuukana uraia wa nchi zao," anasema ofisa huyo.
Anasema operesheni hiyo imefanikiwa kuwaondoa baadhi ya wahamiaji haramu, lakini ukiipima kwa mantiki ya kuondoa wahamiaji wanaosababisha athari kwa mazingira na usalama wa wananchi ni vigumu kusema operesheni imefanikiwa.
"Bila kuwachambua akina nani walipewa uraia kwa kufuata taratibu na kuwachambua upya, hali inavyoonyesha itakuwa vigumu sana mikoa hii ya Kagera, Kigoma na Geita kutulia, tutakuwa tunafanya operesheni kwa gharama kubwa lakini baada ya muda hali inajirudia, tunahitaji kuwachambua hawa watu upya," anafafanua ofisa huyo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Kasulo mkoani Kagera, Yusufu Katula, kijiji kilichoathirika kwa kukaliwa na wahamiaji haramu, anasema baadhi ya wahamiaji haramu wanapitiwa vibali vya uraia bila serikali ya kijiji kushirikishwa.
"Kwa watu ambao tunawajua kabisa kuwa ni wahamiaji haramu na ambao tumewaripoti kwa serikali ni wawili tu ninaweza kusema kwa uhakika wamerejeshwa Rwanda, wengine nasikia wamepewa uraia, sijui kilitokea nini," anasema Katula.
Chanzo chetu kingine kutoka ndani ya Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kagera kilieleza kuwa wapo baadhi ya wafugaji hao matajiri waliokamatwa lakini ilibidi waachiwe kwa sababu walikuwa na vibali vinavyoonyesha ama ni raia au wanaishi nchini kihalali.
Raia Mwema lilipomtafuta Kiongozi wa Operesheni hiyo, Kamanda Simon Siro, Jumatatu wiki iliyopita, alisema hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo hadi Jumatano wiki hii, siku ambayo gazeti hili tayari linakuwa limekwishachapishwa na kusambazwa.
Kwa upande wake kiongozi wa Timu ya Habari na Mawasiliano ya Operesheni Kimbunga, Zamaradi Kawawa, amesema operesheni hiyo ni endelevu na hakuna mtuhumiwa atakayeachwa.
"Napenda kukuhakikishia kuwa operesheni ya kuondoa watu  wanaoishi nchini isivyo halali sambamba na majambazi, majangili, silaha zinazomilikiwa isivyo halali, wafugaji haramu ni endelevu. Tuko katika awamu ya pili ambayo inakwenda hadi Oktoba 20, mwaka  huu. Hakuna mtuhumiwa atakayeachwa bila kuchukuliwa hatua ili kuthibitisha uraia wake na serikali kuridhika na uthibitisho huo," alisema Zamaradi Kawawa.
Wakati operesheni Kimbunga inaanza gazeti hili liliandika habari ya wananchi wa Mkoa wa Kagera kutokuwa na imani juu ya operesheni hiyo na kueleza kuwa kipimo cha mafanikio ya operesheni hiyo itakuwa ni kuona kama wahamiaji haramu ambao pia ni wafugaji matajiri  wataondolewa, huku wakimtaja kigogo mmoja ambaye walisema bayana kuwa kama haitamgusa kigogo huyo, basi haitakuwa na maana.
-raia mwema

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger