muhtasari

Home » , » Serikali yakamilisha tovuti kuwasiliana na wananchi...

Serikali yakamilisha tovuti kuwasiliana na wananchi...

·      
Previous
Left arrow key
Next
Right arrow key
    Close
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue
SERIKALI kupitia wakala wa Serikali Mtandao (EGA) imefanya mapinduzi makubwa ya kuboresha huduma zake kwa kuanzisha tovuti mpya itakayokuwa dirisha huru la kila mwananchi kuihoji wakati wowote na kupata majawabu ya haraka ya kero zao katika sekta yoyote ya umma nchini.
Sambamba na hilo, kila kijiji na mtaa kote nchini kunaandaliwa utaratibu wa kuanzishwa kituo cha teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama) sambamba na kuweka mfumo rahisi wa mawasiliano ya simu zisizo na mtandao wa intaneti ili kuwezesha wakazi wa vijijini kuwasiliana na serikali moja kwa moja.
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue aliyasema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari katika Ofisi za EGA mara baada ya kufanya ziara ya kawaida ya kikazi kujionea utendaji kazi wa wakala huo katika kipindi cha mwaka mmoja tangu ulipoanzishwa.
Wakala huo ulianzishwa Julai mwaka jana (2012). Ingawa hakueleza ni lini hasa tovuti hiyo itazinduliwa rasmi, Balozi Sefue alisema muda mfupi ujao itazinduliwa na kwa sasa ipo katika hatua za mwisho za kukamilishwa.
Alisema maboresho makubwa yanatokana na kuwepo kwa Mkongo wa Taifa unaowezesha huduma moja kutolewa kwa watu wengi kwa wakati mmoja.
Ofisa Mkuu Mtendaji wa EGA, Dk Jabiri Bakari aliwaambia waandishi kuwa hivi sasa tovuti hiyo iitwayo www.tanzania.go.tz ipo hewani na mwananchi anaweza kuingia na kupata taarifa muhimu za serikali ambazo awali hakuwa na uwezo wa kuzipata ili kujibu maswali ya kero zinazomkabili katika eneo lake.
Akitoa mfano wa namna ya utatuzi wa kero, Balozi Sefue alisema, ikiwa wakulima katika eneo fulani mazao yao yamevamiwa na ugonjwa usiojulikana, wanaweza kupiga picha sehemu iliyodhurika na kuituma kwenye mtandao na kisha watapata jibu la aina gani ya dawa watumie kumaliza tatizo bila kuhitaji mtaalamu kufika walipo.
Hata hivyo, Balozi Sefue alikiri kuwepo kwa changamoto kadhaa za matumizi ya Tehama, ikiwemo wizi wa nyaraka za siri za serikali, uhalifu wa mtandao lakini alisema serikali haiwezi kukwepa kutumia teknolojia hiyo, ila cha msingi ni kuweka utaratibu na sheria zitakazowezesha utekelezaji wake.
“Kama mnavyofahamu Tanzania imeingia katika mpango wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership-OGP), mambo yote ya utendaji wa serikali kwa umma yasio siri, yaweze kupatikana, na mifumo hii ikikamilika, kila mwananchi asiogope kutumia kwa uhuru, mfano kuhoji miradi ya maji, kilimo, umeme, kila kitu kitaelezwa na kujibiwa,” alisema Balozi Sefue.
-habarileo

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger