muhtasari

Home » , , » MAKUBWA...MAHARI NDOGO, WAREMBO WA KINYARWANDA WASABABISHA WAHAMIAJI HARAMU NGARA...

MAKUBWA...MAHARI NDOGO, WAREMBO WA KINYARWANDA WASABABISHA WAHAMIAJI HARAMU NGARA...




 
Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta
ONGEZEKO kubwa la wahamiaji haramu wilayani Ngara mkoani Kagera linatokana na Watanzania kuamua kuoa wanawake wa Rwanda kuliko Watanzania kutokana na kutozwa mahari kidogo na kuvutiwa na uzuri wa wanawake wa Kinyarwanda, Imeelezwa.
Katika hatua nyingine Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta ameahidi kuwasilisha ombi maalumu kwa Rais Jakaya Kikwete ili wanawake wa Rwanda waliokuwa wameolewa nchini na kukumbwa na Operesheni Kimbunga, warejee nchini kuungana na familia zao lakini kwa kuhalalisha ukaazi wao.
Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Constatine Kanyasu aliyekuwa akisoma taarifa ya utekelezaji wa Operesheni Kimbunga awamu ya kwanza iliyohusisha mpaka wa Rusumo unaozitenganisha Rwanda na Tanzania, alisema kumekuwepo na ongezeko kubwa la wanaume wa Tanzania kuoa wanawake wa Rwanda kutokana na udogo wa mahari na uzuri wa Wanyarwanda.
Alisema hata hivyo pamoja na kupendezewa na vitu hivyo kwa wanawake wa Kinyarwanda lakini wanaume hao wa Tanzania wanashindwa kuwalipia wake zao hao ada ya Dola za Marekani 550 ( Sh 880,000) zinazotozwa kila baada ya miaka miwili ili kuhalalisha ukazi wao nchini kutokana na kutobadili uraia kuwa Watanzania.
“Waziri (Sitta) sababu kubwa wanayoitoa wanaume wengi wilayani hapa (Ngara) kama sababu ya Watanzania wengi kuamua kuwaoa Wanyarwanda ni kutozwa mahari kidogo sana kuliko ile inayotozwa ili kumuoa mwanamke wa Tanzania. Inasemekana kuna familia wanapokea hadi kuku, mbuzi au fedha kidogo ili kuruhusu mtoto wao kuolewa.
“Kwa vile wanapenda kuwa na wake na kwa vile hawana uwezo wa kifedha wa kutoa mahari kubwa uamuzi wanaofikia ni kuoa wanawake wa Kinyarwanda, lakini kwa kufanya hivyo wanajikuta pia wanashindwa kuwalipia wake zao ada hiyo ya ukazi na kuwafanya kuishi nchini kinyume cha utaratibu,” alisema Mkuu huyo wa Wilaya.
Alisema kutokana na hatua hiyo Operesheni Kimbunga imewakumba wanawake wengi waliokuwa wameolewa nchini hatua iliyosababisha kubakia kwa watoto wasiokuwa na mama wa kuwalea na inayozorotesha uhusiano wa kifamilia na mataifa ya Rwanda na Tanzania.
Alisema wakati maofisa wa Serikali wa pande hizo mbili walikuwa na kawaida ya kukutana kila baada ya miezi mitatu kuzungumzia masuala mbalimbali ya ushirikiano na usalama, tangu kuanza kwa Operesheni Kimbunga vikao hivyo havifanyiki.
Akizungumzia kuondoka kwa wanawake walioacha familia zao, Waziri Sitta ambaye pia alikiri uzuri wa wanawake Wanyarwanda alisema atawasilisha pendekezo kwa Rais Kikwete ili waweze kuruhusiwa kurejea nchini na kufuata taratibu za ukazi halali ili kuweza kulea familia zao.
“Hatuna ubaya na watu wa Rwanda hata chembe na tunaomba walielewe hilo.Operesheni Kimbunga imewakamata pia Wahindi, Wamalawi, Wachina na hawa Wamakonde maana wapo Wamakonde wa Kusini mwa Tanzania lakini wapo Wamakonde wa Kaskazini mwa Msumbiji hawa pia wamekumbwa na operesheni hii.
“Ikumbukwe kwamba ni haki ya kila nchi kuendesha operesheni ya kuhakiki ukazi wa wahamiaji. Ila kwa sababu ya ujirani mwema na hasa kwa kuzingatia hili la wanawake kuacha familia zao nitapeleka mapendekezo kwa Rais tuweze kurekebisha maana tunabanwa pia na mikataba ya kimataifa inayohusu haki za binadamu na watoto,” alisema Sitta.
Akizungumzia malipo ya Dola 550 kila baada ya miaka miwili zinazopaswa kulipwa ili kuwezesha mke asiye raia kuishi nchini, Waziri Sitta alisema ni vizuri kiwango hicho kikaangaliwa upya kutokana na ukweli kwamba wanaume wengi wanaokimbilia Rwanda kuoa wanakwepa ukubwa wa mahari nchini Tanzania kwa kutokuwa na uwezo.
“Nadhani kuna umuhimu wa kuangalia upya kiwango hiki, maana kwa mtu asiye na uwezo kulipa ada hiyo tena kwa Dola ya Kimarekani kunaweza kuwa ni chanzo cha kukwepa sheria na taratibu za nchi yetu. Lengo si kuwafukuza wenzetu bali kuwataka wafuate sheria,” alisema.
Akizungumzia wahamiaji haramu waliorejeshwa makwao, Kamanda wa Uhamiaji Rusumo, Samwel Mahilane alisema hadi kufikia Oktoba mosi mwaka huu, wahamiaji haramu 7, 858 walirejea makwao kwa hiari kupitia mpaka wa Rusumo, huku wahamiaji 2,890 wakirejeshwa kwa nguvu na kufanya jumla ya wahamiaji waliorejea nchini Rwanda kufikia 10,348
-habarile

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger