muhtasari

Latest Article Get our latest posts by subscribing this site

RIDHIWANI: SIASA NINAZOFANYA HAZINA UHUSIANO NA BABA...

 

Ridhiwani Kikwete.Mshindi wa kura za maoni za kugombea ubunge wa Jimbo la Chalinze kwa tiketi ya CCM, Ridhiwani Kikwete amesema siasa anazofanya sasa hazina uhusiano wala ubia na baba yake.
Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kutangazwa kwa matokeo ya kura za maoni za chama hicho katika jimbo hilo kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Msata alisema anafanya siasa kwa maisha yake na si kwa mgongo wa baba yake kwani aliingia katika siasa akiwa na umri wa miaka mitano na hakuwahi kufanya hivyo kwa sababu ya baba yake.
“Siasa ninayofanya haina uhusiano na baba yangu, nafanya siasa kwa maisha yangu na sina ubia na baba yangu katika hili” alisema mtoto huyo wa Rais Jakaya Kikwete.
Akijibu swali la kwa nini amejiingiza katika siasa tofauti na maneno yake aliyowahi kutamka mwaka 2010 kuwa hawezi kushiriki katika kinyang’anyiro cha ubunge katika jimbo hilo, Ridhiwani alisema wakati huo hakuwa tayari.
“Kwenye siasa usiwe muwazi katika kila kitu, ukiwa hivyo unawapa nafasi maadui kukushambulia, mimi hapa Chalinze ni kwetu, kwa wazazi wangu na kule Bagamoyo tunakwenda tu kikazi na ndiyo maana nikaamua kurudi nyumbani kuomba ridhaa. Nashukuru kuongoza katika kura za maoni ninaona ni kiasi gani ninaungwa mkono,” alisema.
Katika kura hizo za maoni Ridhiwani alibuka mshindi kwa kura 758, akifuatiwa na Imani Madega aliyepata kura 335, Ramadhan Maneno (206) na Mkwazu Changwa (17).
Kamati Kuu ya CCM (CC), inatarajiwa kukutana Machi 8, mwaka huu kupitisha jina mgombea wake wa ubunge katika jimbo hilo nafasi ambayo iliachwa wazi na Said Bwanamdogo aliyefariki dunia Januari 22, mwaka huu.
-mwananchi

CCM, CHADEMA, CUF WANAVURUGA BUNGE, ASEMA DOVUTWA…

Mjumbe wa bunge maalumu la katiba Fahmi Dovutwa akichangia mada wakati wa semina ya wajumbe hao ya kupitia vifungu vya rasimu ya kanuni juzi.Picha na Silvan Kiwale 

Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Fahmi Dovutwa alichafua hali ya hewa baada ya kuvituhumu vyama vya CCM, Chadema na CUF kuwa ndiyo vinavuruga Bunge kwa sababu ya misimamo yao.
Hali hiyo ilitokea wakati mjumbe huyo akichangia mjadala wa Rasimu ya Kanuni za Uendeshaji wa Bunge Maalumu la Katiba juzi.
Dovutwa alitoa shutuma hizo baada ya mjumbe mwingine, Julius Mtatiro kueleza kuwa amepitia Rasimu ya Kanuni lakini hakuona mahali panapoeleza mpangilio wa ukaaji wakati wa kupiga kura.
Hali hiyo ilimfanya Dovutwa, kusimama na kutoa tuhuma kuwa baadhi ya wajumbe wamehongwa na kwamba kuruhusu mpangilio maalumu ni kukaribisha mgawanyiko.
Alisema kukaa kwa mpangilio huo kutawapa nafasi viongozi mbalimbali kushinikiza wajumbe wao katika maamuzi ya mambo mbalimbali.
“Ukaaji wa sasa umezingatia masilahi ya nchi, utashi na matakwa ya wananchi. Watu wa CCM, CUF na Chadema ndiyo mnaharibu mkutano (Bunge),” alisema Dovutwa.
Dovutwa alisema vyama hivyo vinatofautiana katika masuala mbalimbali na misimamo yao ndiyo imetawala bunge hilo.
“Mnatulazimisha tuwasikilize nyie tu. Kwa hiyo Mwenyekiti usikubali, kikao hiki kizingatie masilahi mapana ya makundi mbalimbali,” aliongeza Dovutwa.
Baada ya kutamka hilo, mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Kupitia Kanuni, Amon Mpanju alisimama na kumtaka Kificho kulisaidia Bunge hilo kwenda na utaratibu aliowatangazia juzi wajumbe, ambao wanatakiwa kuwasilisha hoja zao kwenye kamati kisha kutolewa uamuzi.
“Naomba uamuzi ukishafanyika, kiti chako kisiruhusu mtu mwingine kuingilia maana mchakato hautafika mwisho. Nawaomba wajumbe wenzangu tusilete michango inayoweza kuleta hisia za mgawanyiko miongoni mwetu,” alisema Mpanju.
Mtatiro alisema hakupendezwa na mchango wa Dovutwa na kutahadharisha ukweli hauwezi kukwepeka kwa kuwa kuna watu wanaotoka katika makundi mbalimbali.
“Wakati wa kupiga kura tunahitaji theluthi mbili ya wajumbe wa Tanzania Bara na idadi kama hiyo kwa wajumbe kutoka Zanzibar kwa hiyo ili kurahisisha kazi hiyo, wajumbe kutoka Zanzibar wakae upande wao na wale wa Bara wakae upande wao,” alisema Mtatiro.
-mwananchi

HATARI…MTOTO ANUSURIKA KIFO BAADA YA KUCHINJWA NA BABA YAKE MZAZI HUKO KAHAMA...

MTOTO ACHINJWA
Mtukio ya kikatili yameendelea kushika kasi wilayani Kahama mkoani Shinyanga ambapo mtoto aitwaye Said Siraji/Said Joshua  amelazwa katika Hospitali ya wilaya usiku wa kuamkia leo, baada ya kunusurika kifo katika jaribio la kuchinjwa na baba yake mzazi aliyejulikana kwa jina la Salvatory.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya wilaya-Kahama; Dakta Joseph Fwoma amesema Siraji amefikishwa hospitalini hapo leo alfajiri baada ya kuokotwa na wasamaria wema akiwa anakimbia huko akivuja damu shingoni.
Dakta Fwoma amesema baada ya kufikishwa hospitalini madaktari walimfanyia upasuaji na kumshona sehemu ya koromeo aliyochinjwa na hadi alasiri hii hali yake imeendelea vizuri hasa baada ya kuongezwa damu. 
Kwa mujibu wa mama mzazi wa Mariamu Idd(35) amesema, Mtoto Siraji jana alichukuliwa na baba yake mzazi anayeitwa Siraji Salvatory(45) kwenda naye kwake mitaa ya Majengo kwa kuwa wazazi hao walikwisha achana siku nyingi.
Mariam amesema, awali Salvatory alikuwa akimchukua Siraji mara kwa mara na kumpeleka nyumbani kwake na baadaye kumrudisha akidai kuchoshwa na huduma za matibabu kutokana na mtoto huyo kuwa na matatizo ya kiafya.
Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema chanzo cha tukio hilo inasadikiwa kuwa mtuhumiwa anaugua ugonjwa wa akili.

"CHADEMA NI CHAMA CHA WAHUNI" ASEMA MWIGAMBA... Asema kitavuruga ndoto za Watanzania Afichua ya Zitto Kabwe na chama kipya


WAKATI maandalizi yote ya uzinduzi wa chama kipya cha ACT-Tanzania yakiwa yamekamilika, Katibu Mkuu wake Samson Mwigamba, ameiponda CHADEMA kuwa ni kusanyiko la wahuni na si wanasiasa.

Amewatahadharisha Watanzania kutokubali kurubuniwa na kauli kuwa CHADEMA ndio mkombozi wa taifa.
 mwigamba
Amesema viongozi wa chama hicho asilimia kubwa wapo kwa ajili ya maslahi binafsi.
“Watanzania wawangalie na ikibidi wawapuuze, nilikuwepo nafahamu kila kinachoendelea, pale hakuna chama licha ya kujinadi kuwa wakombozi wa wananchi, ni waongo wakubwa. 
“Kuna watu wapo pale kwa ajili ya maslahi binafsi na familia zao, hakuna mtanzania atakayetetewa wala kuletewa maisha bora kama watakiweka madarakani,’’ alisema Mwigamba katika mahojiano na gazeti hili jana.

 
Alisema CHADEMA inatumia mabavu na kuchochea vurugu kwa kuwa hakuna kiongozi bora mwenye uwezo wa kuwaongoza wananchi zaidi ya kusheheni viongozi wa matukio na si wa kuwazungumzia wananchi.

 
Mwigamba alisema kupitia chama chao, wamejipanga kuleta mabadiliko ya kisiasa hasa kwa vyama vya upinzani nchini, ambapo alisema muda wowote kuanzia leo, wanatarajia kupewa usajili wa kudumu wa chama hicho.

 
Alisema hawajakianzisha chama hicho ili kuhujumu upinzani, bali kukidhi haja ya watanzania.
Alikanusha uvumi kuwa wanatumiwa na CCM kuvuruga upinzani nchini.
Alisema hayo ni mawazo ya watu wasio na ufahamu mzuri.

 
“Tulikuwa na mipango ya kwenda mkoani Mwanza kufanya mkutano wa hadhara, tumeshindwa baada ya kukosa fedha, ila tutafika kwa nguvu zetu wenyewe mkoani humo na mikoa mingine nchini,” alisema Mwigamba.

 
Akizungumzia madai ya chama hicho kufadhiliwa na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zitto Kabwe, Mwigamba alisema si za kweli.
“Hatufadhiliwi na Zitto na tutasimama kwa nguvu yetu, japokuwa tunamuhitaji na tumeanza naye mazungumzo ili kumuomba ashirikiane nasi katika harakati za kuleta mabadiliko,” alisema Mwigamba.

 
Alisema bado hawajafanikiwa kumshawishi Zitto, licha ya kuwa wamejipanga kuwa na wanasiasa makini wenye mtazamo wa mabadiliko.
“Sheria haziruhusu Zitto kuwa na vyama viwili, yeye ni mwanachama halali wa CHADEMA kwa kuwa ana kesi mahakamani. Kama akipenda kuja aje na asifikirie ubunge wake kwani tunamuhitaji,” alisema.

 
Pia, alisema mbali ya kumshawishi Zitto kujiunga na Chama hicho, walikuwa na mpango wa kumshawishi Dk. Kittila Mkumbo ajiunge na chama hicho, wamekwama.
Alisema Dk. Kittila aliwaambia hataki tena kujihusisha na masuala ya siasa.
Mwigamba na Mkumbo walifukuzwa CHADEMA kwa madai ya kuandaa waraka wa siri waliouita wa mabadiliko ya uongozi uliokuwa ukieleza harakati za kuwang’oa viongozi walioota mizizi.

MATUKIO YA VURUGU YA CHADEMA


Viongozi na wafuasi wa chama hicho wanatuhumiwa kushiriki kwenye matukio ya vurugu ambazo baadhi zimekuwa zikigharimu maisha ya watanzania. 
Vurugu nyingi hutokea kwenye mikutano ya hadhara hasa wakati wa kampeni za uchaguzi.
Kwa sasa wanadaiwa kupeleka makundi ya vijana kutoka mikoa mbalimbali katika jimbo la Kalanga mkoani Iringa, ambako kunatarajia kufanyika uchaguzi mdogo wa ubunge.
Inadaiwa chama kiliingiza silaha mbalimbali jimboni humo vikiwemo visu, mapanga na marungu, ambazo zimekamatwa.

HATARI…MAUAJI YAITIKISA NCHI...JAMBAZI LAENDESHA MAUAJI YA WATU 8 KWA SIKU TATU MFULULIZO, IGP MANGU ASHTUSHWA, APELEKA WAPELELEZI KUMSAKA…


Mauaji ya kutisha yametikisha wilaya ya Tarime kiasi cha kumfanya Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu, kutuma timu maalum kutoka makao makuu ya jeshi hilo inayohusisha kamisheni ya Operesheni kufanya uchunguzi.

Hatua ya kupelekwa kwa timu hiyo inatokana na mauaji ya mfululizo katika mji wa Tarime ambayo ipo kwenye himaya ya Kanda Maalum ya Polisi ya Tarime na Rorya ambayo yametokea kwa watu wanane katika kipindi cha siku tatu.

Mauaji hayo yanadaiwa kufanywa na jambazi mwenye silaha katika mji wa Tarime mkoani Mara kwa siku tatu kuanzia Jumatatu hadi jana.

Mmoja wa watu waliouawa ni askari mstaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Koplo Zakaria Chacha Mwita ambaye ni mtoto wa marehemu Meja Jenerali Mwita Marwa.

Pia wamo aliyekuwa Mhandisi Ujenzi Wilaya ya Rorya, aliyetajwa kwa jina la David Mwasi Misiwa.

Wengine ni mfanyabiashara, Samuel Richard Mohenga na huku Jeshi la Polisi likisema kuwa linaendesha msako.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Tarime/Royra, Justus Kamugisha, alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kusema kuwa mtu anayesadikiwa kuwa jambazi akiwa na bunduki kwa siku tatu kuanzia Januari 26, mwaka huu usiku aliua watu saba kwa kuwapiga risasi  na kujeruhi kadhaa.

Aliwataja wengine kuwa ni mwendesha bodaboda, mkazi wa kijiji cha Nkende, Juma  Marwa Nyaitara, Erick Lucas Makanya, mfanyabiashara  wa bucha mkazi wa kijiji cha Rebu, Juma Mwita Mroni na mkazi wa kijiji cha Kenyamanyori, Robert Chacha Kisiri.

Jana asubuhi, wakazi wa mji wa Tarime na vitongoji vyake walimfananisha mtu aliyekuwa amevaa koti refu na mtuhumiwa wa mauaji hayo na kutaka kumshushia kipigo, lakini aliokolewa na polisi waliorusha risasi hewani na kumpeleka katika kituo cha polisi.

Kamanda Kamugisha aliwashauri wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa mara watakapomuona mtuhumiwa.

 Alisema polisi wanafanya msako katika vijiji vya Kenyamanyori, Rebu, Nkende, Mogabiri na Kibumaye katika kata za Kitare, Turwa na Binagi kwenye Tarafa ya Inchage.

Mkuu wa Mkoa wa Mara, John Tuppa na Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele wakishirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Tarime jana  walitembelea maeneo ya vijiji ambavyo wakazi wake wameuawa na jambazi hilo.

TIMU YA MAKAO MAKUU
Alizungumzia timu iliyotumwa Tarime, Mkuu wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi nchini, Kamishna Paul Chagonja, alisema kuwa ni ya wapelelezi na Intelijensia na inakwenda kuongeza nguvu katika juhudi zinazofanywa na mkoa wa Mara kuhakikisha jambazi huyo anakamatwa ili kuondoa hofu kwa wananchi.

Chagonja alisema juhudi za kumsaka jambazi huyo zinaendelea kufanywa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

SOPHIA SIMBA ALAANI MAUAJI
Wakati huo huo, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba,  amelaani maauji ya wanawake watano waliotaarifiwa kuuawa katika wilaya za Musoma, Butiama na Rorya mkoani Mara.

Alisema wizara inasisitiza kuwa mtazamo huo ni hasi na unakwenda kinyume cha haki za binadamu hivyo jamii haina budi kuachana na imani zinazosababisha mauaji.
 
“Wizara inahimiza wananchi kupinga dhana potofu zinazopelekea mauaji ya wanawake ikiwa ni pamoja na imani za kishirikina, uchu wa kupata utajiri wa haraka, kulipiza kisasi na kuendeleza hulka ya ukatili katika jamii,” alisema.

Alisema: “Mauaji dhidi ya wanawake yanapotokea katika jamii zetu yanarudisha nyuma juhudi za serikali katika kuzuia ukatili dhidi ya wanawake katika jamii kutokana tu na tofauti za kimaumbile.
 
Wizara inaitaka jamii itambue kuwa wanawake wana haki ya kuthaminiwa utu wao na kushiriki haki zote za msingi bila ubaguzi wowote ambao unaweza kuhatarisha haki yao ya kuishi ambayo ndiyo haki kuu kuliko haki zote,” alisema na kuongeza:

“Kushamiri kwa mauaji ya kikatili wanayofanyiwa wanawake katika wilaya za mkoa wa Mara ni jambo ambalo linasababisha hofu kubwa miongoni mwa wanawake. Mauaji hayo yanawakosesha amani na utulivu na hivyo kuzorotesha ari yao katika shughuli za uzalishaji mali.”

CHANZO: NIPASHE

KATIBA MPYA KUTUMIKA KATIKA UCHAGUZI MKUU UJAO...KATIBA YA TANGANYIKA YAPENDEKEZWA IPEWE MAANDALIZI YA MIAKA MINNE...


Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya, imeelekeza kipindi cha mpito ambacho pamoja na mambo mengine, kitaandaa mazingira ya Katiba hiyo kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. 
 
“Kufanya maandalizi na kuendesha Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa kuzingatia masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 2014 na kufanya maandalizi ya mambo yote muhimu kwa ajili ya utekelezaji bora wa masharti ya kikatiba yaliyomo kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 2014,” inasema sehemu ya rasimu hiyo.
 
Tume ya Mabadiliko ya Katiba pia imependekeza kipindi cha mpito cha miaka minne kuanzia tarehe ya kuanza kutumika kwa Katiba Mpya ili sheria zilizopo ziweze kubadilishwa.
 
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alisema jana kwamba katika kipindi hicho cha mpito utakuwa ni muda wa kutungwa kwa Katiba ya Tanganyika. 

Warioba alisema pia katika kipindi hicho, utakuwa ni muda wa mgawanyo wa rasilimali baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali za nchi washirika.
 
“Katika kipindi hicho pia utakuwa ni muda wa kufanya maandalizi na kuendesha Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kwa kuzingatia masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 2014,” alisema.
 
Warioba alisema katika kipindi hicho, Katiba ya Zanzibar itafanyiwa marekebisho ili kuwiana na masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 2014.
 
Sehemu ya Rasimu ya Katiba ya Muungano, imependekeza kuwa maoni yaliyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, yanaweza kutumika kutengeneza Katiba ya Tanganyika.

>>Mwananchi

ZITTO KABWE,KITILA NA MWIGAMBA KUHOJIWA NA CHADEMA IJUMAA YA WIKI HII...



Hatima ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, na wenzake waliovuliwa nyadhifa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), itajulikana Ijumaa wiki hii wakati Kamati Kuu ya chama hicho itakapokutana kuzungumzia sakata hilo na kutoa maamuzi ya mwisho.

Afisa Uhusiano wa Chadema, Tumaini Makene, alisema jana kuwa chama kimewaandikia barua ya kuitwa mbele ya kikao ili wasikilizwe.

Mbali na Zitto aliyevuliwa unaibu katibu mkuu na Naibu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, wengine waliovuliwa nafasi zao ni aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk. Kitila Mkumbo, Novemba 22, mwaka huu kwa tuhuma za kukisaliti chama.

“Chama kimewaandikia barua hiyo baada ya kuwa kimeshawaandikia barua ya kuwajulisha kuwa kimeshapokea maelezo yao ya maandishi kuhusu tuhuma 11 walizotuhumiwa nazo. Kwa hiyo wametakiwa kufika kwenye kikao cha Kamati Kuu Januari 3, mwakani (Ijumaa) ,” alisema.

Makene alisema wameitwa ili wasikilizwe kutoka midomoni mwao kuhusu tuhuma zinazowakabili na kwamba hilo limefanyika kwa mujibu wa kanuni ya uendeshaji chama, katika kifungu cha 6.5.2 (b) na 6.5.2 (d).

Alisema kifungu hicho kinaelekeza kwamba Kamati Kuu inaweza kuchukua hatua za dharura bila kuzingatia utaratibu wa (b) na (c) kama itaona maslahi ya chama kwa ujumla yako hatarini.

“Lakini katika kuchukua hatua hizo za dharura, mwanachama au kiongozi anayelalamikiwa atalazimika kuitwa kwenye kikao husika. Hivyo chama baada ya kupokea maelezo yao ya maandishi sasa wameitwa wajieleze kwa mdomo. Kila kitu kinakwenda kwa utaratibu hapa,” alisema.

Makene alisema tangu mwanzo chama kiliweka utaratibu kwa kuzingatia katiba, kanuni, maadili, taratibu na miongozo ya chama, ndiyo maana ya taasisi. 
 
CHANZO: NIPASHE

HII BALAA...SHANGAZI WATOTO WAFUNGIWA NDANI KWA MIEZI SITA NA SHANGAZI...

 
“TUNAJUA shangazi anatutesa kwa sababu baba na mama wapo mbali, kama wangekuwepo hapa tusingeteswa hivi. Tunamuomba baba, tunamuomba mama kama watasoma habari hii waje watuchukue turudi nyumbani, shangazi anatutesa sana, wala hatukutegemea,” ndivyo alivyoanza kusema mtoto Hassan Yusuf (5) ambaye ni mkubwa kwa wenzake, Hussein Yusuf (5) na Rehema Said (5). 
 
Ikifika mahali mtoto mdogo anasema anawakumbuka wazazi wake kwa sababu ya mateso anayoyapata ugenini ujue ni zaidi ya ukatili, tena ni ukatili wa kutisha.
 

Watoto hao, kwa sasa wanaishi Nzasa ‘A’, Kata ya Charambe, Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam na ndiko walikopatia mateso yote.

MAMBO YALIPOANZA KUTIBUKA
Wiki iliyopita, watoto hao waliokolewa na majirani katika kifungo cha miezi sita ndani huku afya zao zikiwa zimedhoofu kwa kukosa chakula.

Ilidaiwa kwamba, watoto hao Hassan na Hussein ambao ni mapacha na Rehema,  walifungiwa katika banda la shangazi yao aitwaye Asia Bora ambalo ujenzi wake haujakamilika. Wamekuwa wakiishi humo kwa kula mabaki ya vyakula jalalani.

USHUHUDA WA MAJIRANI
Wakizungumza na gazeti  la Uwazi  hivi karibuni, majirani wa nyumba hiyo walimweleza mwandishi kuwa watoto hao wamekuwa wakionekana  nje ya nyumba hiyo mara chache sana wakiwa wanagombania mabaki ya vyakula kwenye jalala.

“Tumekuwa tukiwaona nje mara chache kwenye jalala. Unajua, Asia (shangazi yao) aliwachukua kwa kaka yake, Kijiji cha Namakongoro Kata ya Lihimalyao huko Kilwa mkoani Lindi.
 

“Tukasikia lengo lake aje kuishi nao kwa vile yeye Mungu hamkujalia kupata watoto. Lakini maisha hapo kwake yakawa siyo mazuri kwa kipato kwa mama huyo.
 Mmoja wa majirani hao aliyejitambulisha kwa jina la Aisha Ramadhan yeye alikwenda mbele zaidi kwa kusema:
 
“Hapo awali tulikuwa tukiwaona wakitoka nje na kucheza na watoto wetu huku wakiwa na afya nzuri. Asia akatueleza kuwa ni watoto wa nduguye, amewachukua huko kijijini.

“Baada ya muda fulani tukawa hatuwaoni, tulidhani amawarudisha kwao, lakini kadiri siku zilivyokuwa zinakwenda mbele tukawa tunawaona mara chache wakiwa jalalani wanapigania mabaki ya chakula.
 

“Kuna siku mimi niliwakamata wakiwa wamebeba mfuko wa rambo wenye kinyesi, walikuwa wanakuja kutupa katika maeneo yetu, nikawarudisha nao kwa shangazi yao. Kumbe nyumba wanayoishi haina choo ndiyo maana wamekuwa wakijisaidia kwenye rambo.

“Siku moja walipotoka nje kutafuta chakula jalalani, mimi na majirani wenzangu tuliwauliza wanaishije? Wakatuambia hawapewi chakula na shangazi yao akitoka asubuhi harudi mapema, akirudi inakuwa ni usiku sana wao wakiwa wameshalala.

“Inasikitisha sana kuwaona watoto hawa wanaachwa peke yao kutwa nzima bila mtu wa kukaa nao na wamekuwa wakifungiwa ndani kwa muda mrefu sasa, ila huwa wanakiuka masharti na kutoka kwa ajili ya kutafuta mabaki ya chakula.

Jirani huyo akaendelea kuanika mateso ya watoto hao: “Kwa kuwaonea huruma tumekuwa tukilazimika kuwapa chakula, lakini Asia anaporudi na kugundua hilo anawapiga, kwa hiyo wakawa waoga kuja kuchukua chakula. Mimi niliumia hadi machozi.”

Jirani: “Baadaye wakawa hawaonekani, lakini cha ajabu mara nyingi tukiamka asubuhi tunakuta mifuko ya rambo yenye vinyesi imetapakaa, tukimweleza Asia inakuwa ugomvi.
 

“Siku moja baada ya shangazi yao kuondoka, nilikwenda kuwachungulia ndani, nikawaona wamekonda sana, wamepauka na wamevaa nguo zilizochakaa.

“Nilitokwa machozi, nililazimika kuwaita wenzangu nao walipofika hakuna aliyejizuia kulia. Tukasema hawa watoto watakufa, ndiyo tukaamua kuwaokoa kwa kupeleka taarifa kwa mzee Dadi Salum ambaye ni polisi jamii wa hapa.

POLISI JAMII NAYE ALIA
“Mzee Dadi naye alipofika na kuwaona kwa macho alilia, watu wakaanza kukusanyika, tukawatoa nje watoto, kila mmoja aliwaonea huruma. Tuliwachukua hadi Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Nzasa A.

SHANGAZI MTU ANUSURUKA KIPIGO
“Hatujui ni nani aliyempigia simu Asia, kwani muda mfupi tu tukasikia yupo nyumbani kwake. Uongozi wa mtaa ulimfuata, walipofika, wanawake wenzake hasa wale anaochukua nao mkopo wa fedha benki walitaka kumpiga wakimuuliza pesa anapeleka wapi.

“Hata hivyo aliokolewa na polisi jamii ambao walimchukua na kumweka katika Bajaj na kumpeleka Kituo cha Polisi Mbagala kwenye Dawati la Jinsia na Watoto, watoto nao pia walipelekwa huko.”

Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Nzasa A, Mrisho Salum alikiri kuwapokea watoto hao wakiwa katika hali mbaya kiafya, wakapelekwa polisi. Akawataka wananchi kutokaa kimya mara wanapoona vitendo kama hivyo.

Mwandishi alifika hadi kituo cha polisi na kuambiwa na askari mmoja kuwa mapacha walichukuliwa na mtu aliyejitambulisha kwa jina la Othman Mbwana  aliyedai ni babu yao.

Mbwana alidai kwamba ameamua kuwachukua watoto hao wakaishi nyumbani kwake wakati akifanya mawasiliano na wazazi wao.
 
“Kwanza nitawapeleka hospitali wakatazamwe afya zao, ila nimesikitishwa sana na hali hii, sijajua ni kwa nini watoto hawa wamefikia hatua hii,” alisema Mbwana.

Rehema yeye alichukuliwa na mjomba wake aitwaye Sood Ismail ambaye alidai anakwenda kukaa naye hadi hapo atakapofanya mawasiliano na wazazi wa huyo mtoto, akisema kitendo cha Asia kimeidhalilisha familia.
 
RPC TEMEKE ATUPIA NENO
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Engelbert Kiondo amewataka wananchi kufichua vitendo viovu ndani ya jamii na amewapongeza vijana wake wa ulinzi shirikishi kuokoa maisha ya hao watoto.


Source: Gazeti  la  Uwazi/ Global publisher

PICHA ZA MKUTANO WA CHADEMA MKOANI MWANZA...

Popular Post

 
Support : OBAMA | OBAMA | OBAMA
Copyright © 2013. DiraYaLeo - All Rights Reserved
Template Created by Barakaeli Aremu Published by Dira Ya Leo
Proudly powered by Blogger